Saturday, June 16, 2012

Nani kama Mwl. Julius Kambarage Nyerere (Baba wa Taifa)?

 Picha hii ni ya mwaka 1976

Hakuna kiongozi ama Mwanadamu ambaye anaweza kukosa maadui ama watu wasio mpenda… hakuna Mwanadamu wala kiongozi ambaye anaweza kuishi bila kuwa na mapungufu …hili pia lipo kwa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere!.. wako ambao wanampinga hata sasa ndani ya nchi yake na kama mwanadamu yako aliyokosea.. lakini tunatakiwa kupima kwa wingi wa mema..

Aliongoza harakati za uhuru, kisha kuliongoza Taifa kwa Miaka 24. Taifa lilikuwa halina wasomi ameacha wasomi lukuki wahandisi, madaktari bingwa wa binadamu, madaktari wa falsafa katika fani mbali mbali na ma-profesa. Kulikuwa na mwanya mkubwa sana (gap) kielimu kati ya watu kwasababu ya imani zao...alitaifisha shule za kiimani ili watu wote bila kujali imani wapate fursa ya kusoma kwasababu wakati huo Serikali ilikuwa bado haina uwezo wa kujenga shule kutosheleza mahitaji yaliyokuwepo. Taifa lilikuwa halina chuo kikuu hata kimoja ameacha vyuo vikuu kadhaa, (Wazungu wakiwa wametawala nchi yetu miaka 72 walituacha bila chuo kikuu hata kimoja wala Mtanzania mwenye PHD hata mmoja kama kumbu kumbu zangu ni sahihi), ameunganisha watanzania kwa lugha na upendo. Alikabili wala rushwa na viongozi wazembe .... alijenga amani ya Taifa na uzalendo kwa kila Mtanzania…alipigania Uhuru wa Afrika na Amani ya Dunia.

kwakweli nahitaji kitabu chenye kurasa kwa uchache zisipungue 1,000 kuelezea mazuri ya Mwalimu. Tanzania tunahitaji kumuenzi kwa vitendo. Mungu Ibariki Tanzania

No comments:

Post a Comment