Sunday, January 18, 2015

Serikali imtumie Ray C



JANGA LA MADAWA YA KULEVYA

SERIKALI IMTUMIE VIZURI RAY C

Unapotazama na kutafakari kwa haraka haraka unaona kama si tatizo kubwa, kwasababu ukiangalia huku, ukiangalia kule unaona watu wako katika pilika pilia za maisha yao.  Mimi pia nilikuwa hivyo, sikuwahi kufikiri kuwa tatizo la madawa ya kulevya ni kubwa zaidi ya linavyoonekana mbele ya macho ya watu. Ukweli ni kwamba tatizo hili ni kubwa kwa uzani ambao ukiujua utaogopa.
Nilizoea kuwaona waathirika wa dawa za kulevya na kuwadharau, leo nathubutu kusema kumbe nilikuwa nakosea sana. Natumia fursa hii kuwaomba radhi waathirika wa dawa za kulevya wote na ndugu zao. Nasema hivi kwasababu kwa elimu niliyoipata baadae ingawa wako wengi wanaingia kwa kupenda hata mimi, hata wewe msomaji waweza kujikuta umeingia katika matumizi hayo bila kutegemea.
Mshituko mkubwa na tetemeko la moyo vilinipata wakati nilipopata fusra ya kumsaidia Rehema Chalamila  “Ray C” katika kampeni zake za kuelimisha watanzania juu ya madhara ya dawa za kulevya yeye mwenyewe akiwa shuhuda mkuu wa janga hilo.

Katika kipindi kifupi nilichokuwa na Ray C chini ya Ray C Foundation tulienda pamoja karibu kila mahali kufanya kampeni zetu. Tulitembelea kwenye Shule za Sekondari kuelimisha hatari iliyopo lakini tulienda kwa waathirika wenyewe na kuongea nao.
KAtika kukutana na waathirika mmoja mmoja na vikao vingi ambavyo tulikuwa tukifanya na ndugu hawa, na ziara zangu pale Hospitali ya Mwananyamala nikiongozana na Ray C  vilinifanya nijifunze mambo mengi ya hatari kutoka kwa ndugu hawa mambo ambayo walipitia, mambo ambayo yanasikitisha na hata yaweza kukuliza.
Madawa ya kulevya yanambadilisha mtu kutoka kwenye ubinadamu wa kawaida na kuwa kiumbe mwengine ambaye anahitaji msaada kurudi kuwa mtu wa kawaida badala ya kudharauliwa. Muathirika anakuwa katika mazingira ambayo yeye mwenyewe hawezi kujimudu kuishi bila kuwa katika hali ile ya kupata dawa. Nilielezwa na waathirika wenyewe kuwa siku mtu anapokosa dawa huwa anaumwa na maumivu ya mwili huwa ni makubwa yasiyona mfano.
Aidha nilipata kufahamnu kuwa kuna namnanyingi zinaweza kumuingiza mtu kwenye matumizi ya madawa ya kulevya na lililoniogopesha ni mbinu za wafanya biashara na mawakala wao kutengeneza soko, hapo ndipo hata mtu ambye hakuwa anataka anaeza kujikuta bila kuelewa ameingia kwenye matumizi ya madawa.
Rehama Chalamila “Ray C” alinipa simulizi nyingi za kusikitisha ambazo zaweza kukutoa machozi, namfurahia sana dada huyu kwasababu ni muwazi na ana uchungu mkubwa sana anapoona vijana wanaendelea kuingia kwenye tatizo hilo. Anatamani kama siku moja Tanzania pasiwepo tone la dawa ya kulevya, anatamani kuona siku moja Tanzania hakuna muathirika hata mmoja, anatamani kuona Tanzania siku moja hakuna mtu ameingiza dawa hata mmoja.
Nakumbuka tulipokuwa Mbeya wakati wa maadhimisho ya siku ya kupambana na madawa ya kulevya Dunia, juni mwaka 2014, Ray C alikuwa kivutio cha wengi, na banda letu lilivutia sana wageni kwasababu ya Ray C lakini hilo si kubwa, Ray C alipopanda jukwaani kutoa ushuhuda wake, Aliliza watu. Ingawa mimi mwenyewe ndio nilimwandikia hotuba yake ya ushuhuda taratibu kadiri alivyoendelea kueleza nilijikuta nikitokwa na machozi. 

Ushuhuda wa Ray C unaumiza kwani hata wakani nilipokuwa nikiandika nilikuwa naumia sana, na hata wakati akifanya mazoezi ya kusoma hotuba hiyo nilikuwa nikiumia, lakini niliumia zaidi wakati alipokuwa jukwaani akiisoma nilipogundua kuwa kumbe si mimi tu ninayeumizwa na historia ya kusikitisha ya Ray C baada ya kuangalia viongozi meza kuu wengi wakifutaa Machozi, nilipoangalia upande mwingine kwa watazamaji niliona watu hapa na pale wakifuta machozi.
Katika muda Mfupi niliokuwa nikimsadia nilijifunza jambo moja kubwa kwamba vijana wengi sana wamevutiwa na Ray C na wanamsikiliza. Walikuwa wakitusikiliza kwa namna ya kipekee sana na kila siku idadi ya vijana waliokuwa tayari kuacha dawa ilikuwa ikiongezeka kwa kasi ya ajabu kutokana na hamasa tuliyokuwa tukiwapa.
Huko kwenye shule za sekondari wanafunzi walifurahi na katika mahojiano yam mmoja mmoja walikiri kupata ufunuo mpya na muhimu katika maisha yao. Jambo hili linanivuta leo kufikiria kama kweli Serikali inakusudia kueneza elimu ya athari ya madawa ya kulevya basi Ray C aweza kuwa chombo kizuri cha kufanikisha hilo. Mimi naamini gharama zinazotumika ni kubwa sana lakini ufanisi wake ni mdogo mno, lakini kwa kumtumia Ray C gharama hizo zaweza kuwa na ufanisi mkubwa kupindukia.
Kama mashirika ya simu, shirika la chakula nk yanakuwa na utaratibu wa kuwa na balozi wa huduma za mashirika hayo basi nadhani ni wakati muafanya wa kumteua Ray C kuwa balozi katika maapambano dhidi ya madawa ya kulevya hasa katika uelimishaji jamii. Kuna mafungu mengi yanatengwa kwenye Serikali na wanalipwa watu ambao kazi zao hazina mchango mkubwa sana kwa Taifa, Serikali ifanye sasa hivyo kwa mtu ambaye ushiriki wake utapanua ufanisi wa malengo ya Serikali kwa kasi kubwa.
Nasema haya kwasababu mimi mwenyewe nimeshuhudia hamasa kubwa ambayo vijana walikuwa wakipata tulipokuwa kwenye kampeni zetu.
Mungu Ibariki Tanzania
Kwa maoni: malihoja@yahoo.com

No comments:

Post a Comment